Thursday, July 17, 2025

Je Nini Chanzo Cha Kauli Mbiu Ya ONE TERM (WANTAM) Nchini Kenya?

Kauli mbiu ya "One Term" au "WANTAM" imeibuka kama wito wa kisiasa unaoashiria kutoridhika kwa wananchi na utawala wa sasa wa Rais William Ruto, wakitaka asihudumu kwa muhula wa pili Mpaka mwaka 2027. Hii inaashiria mabadiliko makubwa katika siasa za Kenya kuelekea uchaguzi wa 2027.


Zifuatazo Ni Sababu Za Kauli Hii Kuhusu Siasa Za Kenya Kuelekea 2027

17 July 2025
Na Mathayo Tajiri Mollel.
Arusha Tz.

🔗. Kukosekana kwa Uaminifu kwa Serikali ya Ruto.
HIi inaweza kuwa sababu kuu, wananchi wengi wamepoteza imani na serikali kutokana na ahadi nyingi zilizoahidiwa na serikali ya Kenya Kwanza (KK) ambazo Mpaka Sasa mpango wa utekelezaji hamna, ongezeko la ushuru, na ukandamizaji wa maandamano ya amani. Hali hii imeongeza wito wa kauli hii ya "One Term" miongoni mwa wapiga kura wengi Nchini Kenya.

🔗. Uasi wa Kizazi cha Gen Z.
   Vijana wa kizazi cha Gen Z wamekuwa mstari wa mbele katika maandamano ya kidijitali na ya mitaani, wakipinga ukandamizaji wa haki za kiraia na ukosefu wa fursa za kiuchumi. Hii inaonyesha mabadiliko ya nguvu za kisiasa kuelekea kizazi kipya. Serikali ya Kenya imekuwa ikitafuta njia ya kuongea na vijana wa kizazi cha Gen-z bila mafanikio kwa kuwa vijana wamegura na kukataa maongezi yoyote na serikali.

🔗. Uwezekano wa Wapinzani Wapya
   Kando na vijana wa kizazi cha Gen-z kuibuka wakiwa na nguvu kubwa katika kuendesha mabadiliko haya ya serikali Nchini Kenya, kuna Majina mapya kama Jaji Mkuu Mstaafu David Maraga, Waziri wa zamani wa mambo ya ndani Fredi Matiangi, yameanza kutajwa kama wagombea wa urais, wakiahidi uadilifu na mageuzi ya kweli. Hii inaweza kuvuruga hesabu za kisiasa za vyama vikuu katika uchaguzi mkuu Wa 2027. Pia itachochea kauli ya (WANTAM) Kupata nguvu zaidi ikididiza ndoto za rais Ruto Kuendelea na awamu ya pili.

🔗 Uteuzi wa Tume Huru ya Uchaguzi (IEBC)
   Rais Ruto ameteua makamishna wapya wa IEBC, hatua inayozua wasiwasi kuhusu uhuru wa tume hiyo na uadilifu wa uchaguzi ujao. Hili nalo litaendelea kuibua mjadala mkubwa mno ambao utaamsha hasira ya vijana kuendelea kuimba wimbo wa (WANTAM).

🔗 Mgawanyiko Ndani ya UDA
   Chama tawala cha UDA kinakabiliwa na migawanyiko ya ndani, hasa baada ya Rais Ruto kumfukuza aliyekuwa Naibu wake Rigathi Gachagua na wandani wake wote, hali imeweza kudhoofisha chama tawala cha UDA na itaadhiri sana kampeni zao za 2027. Kwa sasa Bwana Rigathi Gashagua ameanzisha chama chake kipya kinachoitwa DCP ambacho kinaungwa mkono sana Central Kenya na kwingineko.


🔗 Uhamasishaji wa Vijana na Makundi Maalum
   Mashirika ya kiraia yanahamasisha vijana, wanawake, na watu wenye ulemavu kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi, ikiwa ni pamoja na kujiandikisha kupiga kura na kugombea nafasi za uongozi. Hili ni jukumu ambalo wakenya wengi wamelichukulia kwa uzito mkubwa sana ili kutimiza ahadi waliyojiwekea ya (WANTAM).


Kuna mazungumzo kuhusu mageuzi ya kikatiba kabla ya 2027, ikiwa ni pamoja na mabadiliko ya mfumo wa utawala na ugatuzi(serikali ya majimbo), ambayo yanaweza kuathiri mwelekeo wa siasa za kitaifa.

Kwa ujumla, siasa za Kenya kuelekea 2027 zinaonyesha mabadiliko makubwa, huku wananchi wakitaka uwajibikaji zaidi, usawa, na uongozi wa kweli. Kauli mbiu ya "One Term" ni ishara ya kutoridhika kwa wananchi na wito wa mabadiliko ya kweli katika uongozi wa taifa.

Mathayo Mollel
+254721700996
+255758768243

Sunday, May 17, 2015

BUNGE LAGEUKA UWANJA WA MIPASHO. MAKALA

BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
Kwa takriban wiki moja sasa, Bunge la Jamhuri ya Muungano limegeuzwa uwanja wa kampeni za uchaguzi na watunga sheria wetu wametumia nafasi yao kuonyesha ustadi wao katika mipasho.

Ni Bunge ambalo wananchi wengi waliotaka kulifuatilia walikuwa ni wale waliotaka kusikia vichekesho na ufundi wa kuzima hoja muhimu na kuzifanya kuwa vitu visivyo na manufaa kwa Taifa.

Hayo yote yalitokea wakati Bunge lilipokuwa likijadili Hotuba ya Makadirio na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo imeomba Sh5.8 trilioni, sawa na zaidi ya robo ya bajeti nzima ya Serikali ya mwaka 2015/16 ambayo ni Sh22.4 trilioni.

Hotuba hiyo ilizungumzia zaidi mafanikio ambayo Serikali ya Awamu ya Nne imeyapata katika kipindi cha miaka 10 na haikujikita sana katika kuangalia vipaumbele ambayo Serikali imeviweka kwa mwaka 2015/16.

Jambo kubwa ambalo limeonekana kuwa dhahiri ni jinsi ambayo Serikali ilishindwa kupeleka fedha Tamisemi, ambayo ndiyo inachukua shughuli nyingi za wizara hiyo kutokana na ukweli kuwa inahusika na Serikali za Mitaa na Tawala za Mikoa.

Imedhihirika kuwa katika mwaka wa fedha wa 2014/15 Serikali ilipeleka siyo zaidi ya asilimia 20 kwa Tamisemi, kitu ambacho kilisababisha miradi mingi ya maendeleo isitekelezwa kwa kiwango chake. Au kwa maana nyingine bajeti hiyo haikumgusa mwananchi kwa kuwa wizara iliyo karibu naye haikupewa angalau nusu ya fedha zilizopangwa kwa ajili ya shughuli za maendeleo.

Kwa kuwa wabunge ni wawakilishi wa hao wananchi, tulitegemea eneo hilo ndilo ambalo lingekuwa msingi mkuu wa mjadala. Tulitegemea waheshimiwa wabunge wangehoji sababu za Serikali kutoipa Tamisemi fedha za kutosha kutekeleza miradi ya maendeleo na nini kifanyike ili udhaifu huo uendelee.

Hata hivyo, kilichotokea ni tofauti. Wabunge waliohoji sababu za Serikali kutoipa Tamisemi fedha za kutosha, wakageuzwa kuwa wanakichokonoa chama na serikali yake na badala ya hoja zao kujibiwa, wakatafutiwa udhaifu wao na ndiyo ukawekwa mbele katika mjadala.

Matokeo yake, mjadala ukapoteza mwelekeo na mambo ya msingi kuhusu maendeleo ya wananchi yakawekwa kando.

Hili linaonyesha dhahiri kuwa wawakilishi wetu hawathamini kodi za wavuja jasho zinazowaweka mjini Dodoma kwa takriban siku 44 ili wajadili maendeleo yao.

Hata mahudhurio yamekuwa ni ya chini na wanaokuwapo ndani ya Ukumbi wa Bunge ni wale wanaosubiri nafasi za kuchangia, wengine wanaendelea kutumbua posho majimboni mwao au sehemu nyingine.

Alipoulizwa kuhusu vitendo hivyo, Naibu Spika Job Ndugai alisema ni vigumu kudhibiti wabunge kufanya kampeni wakati wa kuchangia kwenye mijadala ya hotuba za bajeti, hasa wakati huu wa kuelekea Uchaguzi Mkuu.

Ndugai anamaanisha kuwa hawa wabunge hawakupata nafasi ya kufanya kampeni majimboni mwao kwa kipindi chote bcha miaka mitano waliyokuwa ndani ya chombo hicho cha kutunga sheria.

Au kwa maana nyingine, Ndugai anatueleza kuwa hali itakuwa hivyo kwa siku zaidi ya 30 zilizobaki kwa kuwa hiki ni kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu na wao kama viongozi hawataweza kuwadhibiti.

Hatudhani kuwa kauli hiyo ni sahihi na hatuamini kuwa wabunge hawana nafasi nyingine ya kupiga kampeni zaidi ya kipindi hiki.

Tunaushauri uongozi wa Bunge ukune kichwa kuangalia ni kwa jinsi gani itaweza kudhibiti tabia hii na tunaendelea kuwashauri wabunge watambue umuhimu na majukumu yao katika Bunge la Bajeti na kuwatendea walipa kodi kile wanachostahili.


Toka Swahili Hub.

Tuesday, April 28, 2015

Mwana Chama Wa Al-shabab Aliyepanga Kulilipuwa Bunge La....


POLISI wanamzuilia mfanyakazi wa bunge Bwana Ali Abdulmajid baada ya ripoti ya ujasusi kumhusisha na njama ya kundi la Al-Shabaab kulipua Bunge. 
Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya kutathmini hali, kundi hilo la kigaidi pia linasemekana kupanga kushambulia soko la Muthurwa, makanisa ya Nairobi Pentecostal Church, Holy Family Basilica, St Andrews PCEA, na Chuo Kikuu cha Nairobi.
Ripoti hiyo ambayo hutayarishwa na Mkuu wa Polisi wa Nairobi Central, Bw Paul Wanjama, ilimuagiza afisa mkuu msimamizi wa kituo cha polisi bungeni, Samson Chelugo, aimarishe usalama.
Ripoti hiyo iliyoandikwa Aprili 23 ilisambazwa sana Jumatatu katika mitandao ya kijamii.
Iliongeza kuwa mshukiwa huyo anayefanya kazi Bunge la Seneti anahusishwa na msikiti wa Riyadh eneo la Pumwani, ambao awali ulitajwa na ripoti ya Umoja wa Mataifa kama mmoja wa misikiti inayotumiwa na kundi hilo la kigaidi.
Mwekahazina wa msikiti huo Dkt Iddi Waititu Abdallah aliambia Taifa Leo kwamba Bw Ali Abdulmajid aliitwa na polisi Jumapili na akakamatwa na kufungiwa kituo cha polisi cha Kilimani baada ya kujiwasilisha kwao.
Alipuuzilia mbali ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa na kusema msikiti huo hauna uhusiano na  Al-Shabaab.
“Al-shabaab wametuma majasusi wa Amniyat kupanga mashambulio makubwa katika nchini katika siku mbalimbali. Nairobi maeneo yanayolengwa ni pamoja na Bunge kwa kuweka bomu majengo ya Bunge. Kundi hili linapanga kutumia mtu aliye na ushirika na msikiti wa Riyadh wa Pumwani na ambaye ni mfanyakazi wa Seneti kufanikisha shambulio hilo,” ripoti hiyo ya polisi ilisema.
Amniyat ndicho kitengo cha Al-shabaab kinachohusika katika kukusanya habari za kijasusi na kutekeleza mashambulio ya kujitoa mhanga.

Friday, February 20, 2015

Picha Mbalimbali Kutoka Katika Mkutano Wa marais Wa Afrika Mashariki. Kwa hisani ya Mchimba Riziki Media

Marais Wa Afrika Mashariki Kutoka Kushoto Ni Mh.Pierre Ngurunzinza Wa Burundi,Mh.Jakaya Mrisho Kikwete Wa Tanzania, Mh.Uhuru Muigai Kenyatta Wa Kenya, Mh.Yoheri Museven Wa Uganda na Paul Kagame Wa Rwanda Leo Hii Jijini Nairobi

Rais Paul Kagame Na Hasimu Wake Rais Kikwete Na Mwenyeji Wa Rais Uhuru Wa Kenyatta Kabla ya kikao

Rais Wa Kenya Uhuru Muigai Kenyatta Akimkabidhi Rais Wa Tanzania Mh. Jakaya Mrisho Kikwete Uwenyekiti wa Jumuia ya Afrika mashariki Leo Hii Jijini Nairobi.
Mh.Uhuru Kenyatta akimpokea Mh Kikwete Jijini Nairobi



Rais Wa Kenya Uhuru Akimpokea Rais Wa Uganda Mh. Mseven 

Baadhi ya Marais Wa Jumuiaya ya Afrika Mashariki Wakiwa pamoja na makamu wa Rais wa Kenya Mh.Ruto Kabla ya Mkutano


Uhuru Kenyatta Akiwa Makini Kuskiliza Speech Mkutanoni.


Rais Uhuru Na Pierre Ngurunzinza Wakisalimiana


Rais Uhuru Kenyatta Wakisalimiana na Paul Kagame
Picha ni kwa hisani kubwa ya Mchimba Riziki Media.

Tuesday, February 17, 2015

Umaarufu Huu Utaleta Majonzi Tanzania. Tunangamizwa Na Siasa Chafu Kwa Kukosa Maarifa.

Kuanzia mapema mwaka jana wa 2014 chama tawala cha CCM na Msajili wa vyama vya siasa nchini Tanzania wameshindwa kwa pamoja kumchukulia hatua Mh.Edward Ngoyai Lowassa Aliyetangaza nia ya kugombania Urais kupitia chama tawala CCM. Mh. Lowasa ametembea nchi nzima akitoa misaada mbalimbali makanisani na misikitini pia kupiga kampeni kabla ya wakati.Kiukweli mimi ninaona hapa CCM na Mh. Lowasa wanadhihirisha na kuturudisha katika enzi zile; eti bado tuko kwenye chama kimoja. Mbaya zaidi, katika tafrija moja ya kutoa shukrani mwaka jana kanisani Monduli Lowasa alitangaza nia wasi wasi kuwa atagombania urais na hakuna yeyote aliyewahi kumuonya juu ya kitendo kile. Waziri mkuu huyu wa zamani aliyejiuzulu alinistaajabisha pale anapozunguka nchi nzima kujinadi watu wasimame wahesabiwe ili ndoto yake itimie.

CCM wanaonesha kutojali kabisa uwepo wa vyama vingine vya siasa hasa katika suala la haki sawa za mchezo wa kisiasa. Hii inanikumbusha moja ya tawala dhalimu zilizopita miongo kadhaa huko Jamhuri ya watu wa China: mwanamapinduzi—De Xio Peng—alipokuja na kauli mbiu: “Haijalishi kama paka ni mweusi au mweupe bali kama anaweza kukamata panya”. Ni mbinu ya kidhalimu na kizandiki isiyojali sheria na taratibu za mchezo haki kisiasa zinatumiwa na chama tawala. Ili mradi mgombea wao atangazwe kwa wananchi katika staili ya kupiga kampeni kwa kutumia rasilimali za serikali naweza kuhisi.

Baadhi ya magazeti yalifananisha na mikutano ya kuimarisha chama ambayo inafanywa pia na vyama vingine kila siku. Lakini mimi najiuliza: nimeona mheshimiwa Lowasa akijitambulisha na kutambulishwa na wanaojiita Watiifu wa Lowasa, Wanasiasa wengi wanamkumbatia Lowasa tena kutoka chama chake cha CCM. Panakuwepo na lundo la askari karibu wa kila aina, utaona rasilimali mbalimbali za serikali pale na hata baadhi ya viongozi wa asasi za serikali. Haijalishi hiki ni chama tawala ila kama nikifananisha na mikutano ya uimarishaji chama ya hivi vyama vya siasa vya upinzani naona kabisa hakuna usawa.

Nafikiri kipindi cha kampeni kila chama kinapewa fungu la shughuli hiyo na angalau kunakuwa na usawa ambao nafikiri msajili kauona. Nimesoma matangazo mengi yenye salam za pongezi kwa mheshimiwa Lowasa; haya yanatolewa na makampuni, mashirika, na hata idara za serikali. Mwanasiasa ama mwanaharakati kama mimi  akihoji anaonekana kama mwehu na vyombo vya habari. Hakuna chombo chochote cha habari kilichoandika juu ya athari za kitendo hiki cha pongezi kutoka taasisi mbalimbali. Uwezekano wa michezo michafu kati ya mgombea anayepongezwa na asasi zilizompongeza tuutizame iwapo atachaguliwa. Vyombo vya habari labda kwa minajili ya kupata fedha za matangazo vimeona hii itawaathiri kimapato. Uandishi makini upo hapa kweli? Wapi magazeti ya serikali, television ya serikali na radio ya serikali zote zinazungumzia maendeleo ya ccm na Lowasa pekee. Labda nimtahadharishe msajili wa vyama vya siasa aionye CCM na Lowasa dhidi ya tabia ya kuturudisha katika enzi ya chama kimoja ambapo haya yanayotokea ilikuwa ni utamaduni.

Yanayoandikwa sana na magazeti hapa ni juu ya kutabiriwa ushindi wa kizilzala—yaani Tsunami wa mheshimiwa Lowasa. Changamoto kwa vyombo vyetu vya habari ni hii: jamani hivi hamwoni huu ni wakati wa kuwakumbusha watanzania—wadanganyika—juu ya mengi yaliyotokea katika muongo huu unaokwisha wa mheshimiwa Kikwete? Kwa mfano, ile habari ya umeme ya IPTL, mkataba wa Network Solution, Escorow,RichMond pamoja na huu uvunjaji wa mkataba kati ya serikali na kampuni ya City Water kama dhihirisho la utendaji mbovu ambao wananchi wanapashwa waeleweshwe kwa kina ili waweze kuitumia kura yao kwa utashi makini?

Upinzani wetu ni dhahiri ni hoi ila ni lazima tuhakikishe katika serikali ijayo ya CCM wale wote waliohusika kwa njia moja au nyingine hawapewi dhamana tena ndani ya serikali. Katika madhila nilizotaja hapo juu ni wazi wapo mawaziri au hata wabunge; ni jukumu la vyombo vya habari kutoa habari za upelelezi za kina juu ya matukio hayo kwa wananchi ile nao wawajibishe kupitia kisanduku cha kura hapo mwishoni mwa octoba.

Nimegundua kwamba CCM kutuletea mgombea Maarufu imefunika rekodi zote chafu za CCM. Vyombo vya habari naviona vimeamua ‘kufunika kombe mwanaharamu apite’. Japo vyama vya upinzani viko hoi taabani, lakini ipo haja ya ukosoaji unaozingatia haki. Kwani ni wazi kama CCM ingekuwa safi tungetarajia nchi yenye maendeleo makubwa kuliko sasa. Nasema hivi kwasababu nchi ya Uganda pamoja na kuwa vitani kwa muda mrefu iko karibu sawa kiuchumi na nchi yetu. Hatutofautiani sana, nashindwa kuelewa sisi na amani yetu ya muda mrefu kunani jamani? Wanahabari amkeni jamani, igeni wenzenu kwa mfano wa Nation Media na The Standard wa Kenya, The Monitor, Vision na The Observer wa Uganda. Wanakosoa kwa manufaa ya umma.

Mchimba Riziki Kwa swali au Maoni niandikie
Barua pepe: mchimbariziki@gmail.com
Whatsapp: +254715323229

Friday, December 5, 2014

2017 Haitafika Bila Taji "Arsen Wenger" Anena

Kocha wa klabu ya Arsenal, Arsene Wenger ana imani anaweza kuongoza vijana wake kunyakua taji la ligi kuu kabla ya kandarasi yake kuisha mwishoni wa msimu wa 2016/17.

Arsen Wenger

Imani yake ya msimu huu ilipigwa jeki hata zaidi na ushindi wao mwembamba wa 1-0 dhidi ya Southampton Jumatano usiku na hivyo kuzidi kumpa moyo licha ya kuwa wangali katika nafasi ya sita kwa alama 23, ikiwa ni pointi 16 nyuma ya viongozi Chelsea.

Timu hiyo imeandikisha mwanzo wao mbaya zaidi katika ligi ya EPL tangu 1982 na wamejikuta nyuma mno kwa pengo hilo kubwa la alama ikilinganishwa na muhula uliopita ambapo hadi kufikia wakati huu walikuwa uongozini kabla ya kufifia kufikia mwisho wa kampeni na kunusurika kwa kumaliza wa nne.
“Kuna ushindani mkubwa Uingereza na Chelsea wameanza vyema, hilo tunakubali. Itakuwa vigumu kuwafikia lakini kila mmoja atapigania kuwalaza sisi pia tukiwemo. Huwezi kusema kuwa harakati za kuwania taji zimekwisha baada ya mechi 14 pekee tulizocheza hadi kufikia sasa,” Wenger akasema.
“Hatukuanza vyema msimu huu ila usisahau kwamba hatukuwa na kikosi chote pamoja tangu musimu kuanza kwani ulifuatia Kombe la Dunia. Ni lazima tupambane  ili kurudia uwaniaji wa taji kwa haraka katika kila mechi,” akajitetea.

Licha ya yote, Wenger anaonekana kuwa kakalia kuti kavu baada ya mashabiki kuanza kumshurutisha aondoke kama ilivyoshuhudiwa wikendi iliyopita kwenye ushindi wao wa 1-0 dhidi ya West Brom.

Kesi Ya Uhuru Kenyatta Imetupiliwa Mbali.

Wakenya Wakionyesha Furaha Baada Ya Uhuru Kufutiwa Kesi
Habari zilizofika mapema hivi leo zinasema mwendesha mashitaka wa mahakama ya kimataifa ya uhalifu ICC Fatou Bensouda, ametupilia mbali mashitaka dhidi ya Rais wa Uhuru Kenyatta wa Kenya.
Mapema wiki hii mahakama ya kimataifa ya uhalifu  ICC ilimpa wiki moja mwendesha mashitaka huyo kuongeza  kasi ya uchunguzi ama kuyatupilia mbali mashitaka dhidi ya Rais Kenyatta.
Mh.Uhuru Kenyatta
Kesi hiyo iliahirishwa mara kadhaa na mahakama hiyo ya The Hague, na Jumatano ilisema kwamba kuchelewa zaidi kungeweza kuwa kinyume na maslahi ya haki katika mazingira yaliyokuwepo.
Rais Kenyatta alikabiliwa na mashitaka dhidi ya ubinadamu akishutumiwa kupanga ghasia za  baada ya uchaguzi mwishoni mwa mwaka 2007 na mapema 2008. Ghasia hizo zilisababisha vifo vya watu 1,100 huko Kenya na kuwakosesha makazi wengine zaidi ya nusu milioni.
Rais Kenyatta mara kadhaa amesema yeye hana hatia.

Saturday, September 6, 2014

Mwanaume Mmoja Afunga Ndoa Na Maiti..... Ni Wapi Fuatana Nami Mchimba Riziki Nikujuze


MWANAMUME alishangaza familia yake, marafiki na wanakijiji alipoamua 'kufunga’ ndoa na marehemu mkewe katika kijiji cha Kadzinuni, tarafa ya Kikambala, Kaunti ya Kilifi wakati wa mazishi yake.

Kiti Mwangudza Chilango aliamua kutimiza ahadi aliyokuwa amempatia mkewe miaka michache iliyopita kwamba wawili hao wangefunga ndoa rasmi.

Akiwa amevalia suti, Bw Chilango alisimama kando ya jeneza la mkewe akiwa pamoja na msafara wa wasimamizi wake sawa na jinsi inavyofanyika wakati wa harusi.

Pia kulikuwepo na keki ambayo aliikata na kisha ikagawanywa kwa waombolezaji kabla ya mwili kuzikwa.

Kulingana na rafiki wa karibu wa marehemu, Bi Mbeyu Mbura, Bw Chilango alikuwa amemuoa kwa kitamaduni lakini mkewe alikuwa akishinikiza wafanye harusi kanisani.

Bi Mbeyu alifichua kuwa marehemu ambaye alikuwa akiugua ugonjwa usiojulikana alikuwa amemtaka mumewe aape kuwa atamheshimu kwa kumfanyia harusi awe hai ama akiwa amekufa, na ndio sababu mumewe hakuwa na namna nyingine ila kutimiza ahadi hiyo.

“Tunahofia kuwa kitu kibaya huenda kikatokea kwa mumewe ama familia ikiwa ombi la marehemu halitatimizwa. Mumewe anaweza hata kufa,” alieleza Bi Mbeyu.

Mzee wa kijiji Kai Mwandeje alisema kuwa hakuna jambo kama hilo limewahi kutokea eneo hilo na kusema kuwa kitendo hicho huenda kikaleta matatizo mengine baadaye ikiwa mume ataamua kuwa anataka kuoa tena katika siku za usoni.

“Kuvalia mavazi ya harusi kunamaanisha kuwa roho ya mume tayari imeunganishwa na ya marehemu. Itakuwa vigumu kuoa tena isipokuwa kama ahadi hiyo itavunjwa,” alisema Bw Kai.


Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score