Saturday, October 19, 2013

Uharamia Bado Ni Tishio Pembe Ya Afrika


Mashambulizi mawili ya kiharamia wiki iliyopita kwenye upwa ya Somalia yamezusha wasiwasi kwamba kitisho cha uharamia kwenye Pembe ya Afrika hakijaisha, liliripoti jarida la Seatrade Global siku ya Jumatano (tarehe 16 Oktoba).

Ijumaa iliyopita, maharamia waliokuwa kwenye mashua mbili waliirushia risasi meli ya mafuta inayopepea bendera ya Hong Kong, MV Splendor, likiwa ni tukio la kwanza la aina hiyo tangu mwezi Aprili, kwa mujibu wa Shirika la Ujasusi wa Baharini la Dryad lenye makao yake nchini Uingereza. Siku nne baadaye, genge hilo hilo la maharamia liliishambulia meli nyengine kubwa umbali wa maili 270 za majini kutoka mahala yalipotokea mashambulizi ya awali.

"... Mashambulizi hayo dhidi ya meli mbili ndani ya kipindi cha siku nne yanathibitisha kwamba biashara ya uharamia ya Somalia bado haijavunjwa," alisema Ian Millen, mkurugenzi wa upelelezi wa Dryad.

Millen alisifu hadhari na utaalamu wa timu ya walinzi wa MV Splendor katika kukabiliana na mashambulizi hayo, ambapo walifanikiwa kukinusuru chombo, na kuzitolea wito meli nyengine kwenye eneo hilo kudumisha viwango vya hali ya juu vya ulinzi.

Hata hivyo, uharamia kwenye bahari uko kiwango cha chini kabisa katika kipindi cha miaka saba, liliripoti Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Baharini (IMB) siku ya Alhamisi. Kwenye upwa wa Somalia, kulifanyika mashambulizi 10 ya kiharamia katika miezi tisa ya mwanzo ya mwaka huu, ikilinganishwa na mashambulizi 70 kwenye kipindi kama hiki mwaka 2012, ilisema IMB.

"Jukumu kubwa linalotekelezwa na wanajeshi wa majini kwenye upwa wa Somalia halipaswi kudharauliwa. Kuwepo kwao kunahakikisha kwamba maharamia hawafanyi kazi zao wakiwa na hisia za kutokuchukuliwa hatua kama mwanzoni," alisema Mkurugenzi wa IMB, Pottengal Mukundan.

"Ingawa idadi ya mashambulizi imeshuka kwa ujumla, kitisho cha mashambulizi kingalipo, hasa kwenye bahari ya Somalia na Ghuba ya Guinea," alisema. "Ni muhimu kwamba manahodha wa meli waendelee kuwa na hadhari wanapopita kwenye bahari hizi."

By Mchimba Riziki

Uganda Yatishiwa Nayo Kushambuliwa Na Magaidi Waliishambulia Kenya

Kampala,Uganda
Magaidi walioishambulia Kenya na Kutishia kuivamia Tanzania na Rwanda sasa waigeukia Uganda ,hapo jana walitoa vitisho balaa kuhusina na suala la kutaka kuivamia Uganda saa yoyote ile. Jeshi la Uganda nalo lipo Rada kuwathibiti wasifanikiwe kufanya shambulizi lolote na kuleta hasara

Uganda ilikuwa kwenye hali ya tahadhari siku ya Ijumaa (tarehe 18 Oktoba) kutokana na hofu za mashambulizi kama yale ya al-Shabaab katika jengo la Westgate jijini Nairobi, ambako bado wapelelezi wanaendelea kufukua miili iliyooza takriban mwezi mzima baadaye, liliripoti shirika la habari la AFP.

"Kuweni na tahadhari na chunguzaneni hatua na matendo ya kila mmoja, kwani bado tunatishwa na ugaidi," ulisema ujumbe wa polisi ya Uganda, huku vikosi vya usalama vikifanya doria nje ya maduka kwenye mji mkuu, Kampala.

Hatua hii ilifuatia ujumbe wa siku ya Jumanne kutoka ubalozi wa Marekani nchini Uganda ambao ulisema ubalozi huo ulikuwa ukiendelea "kutathmini ripoti kwamba mashambulizi kama yale ya Westgate yatatokea mjini Kampala hivi karibuni". Ubalozi huo ulisema hakukuwa na taarifa zaidi juu ya wakati na mahala wa mashambulizi yoyote.

Siku ya Alhamisi, wapelelezi walipata fuvu la kichwa lililoharibika kwenye mabaki ya jengo la Westgate, walisema polisi wa Kenya, wakiongeza kwamba kipimo cha DNA kitafanywa ili kusaidia kulitambua. Bunduki pia zilipatikana.

Shirika la Msalaba Mwekundu nchini Kenya linasema kuwa watu 23 walipotea baada ya kuzingirwa kwa jengo hilo.

Kuna wasiwasi mkubwa kwamba al-Shabaab watatekeleza kitisho chao cha kufanya mashambulizi zaidi, baada ya wanamgambo hao wenye mafungamano na al-Qaida kusema kupitia mabango kwenye maandamano nchini Somalia kwamba "Westgate ulikuwa ni mwanzo tu."

Mkanda wa vidio ya propaganda pia ulitolewa wiki hii na al-Shabaab ukikipongeza kikosi chake cha wapiganaji wa kigeni, ukionesha waasi kadhaa ambao wanadaiwa kuwa walitoka Uingereza na waliouawa kwenye mapigano.

Hapana shaka, vidio hiyo ilifanywa kabla ya mashambulizi ya Westgate kwani haizungumzii mashambulizi hayo, ingawa inataja juu ya "mateso ya Waislamu nchini Kenya" na pia kwenye nchi nyengine.

Vidio hiyo inayosimuliwa na mwanamme aliyevalia sare ya kijeshi na uso wake ukiwa umezibwa kwa kitambaa na anayezungumza lafudhi ya Kiingereza safi, inadai wapiganaji kutoka mataifa kadhaa ikiwemo Ethiopia, Eritrea, Lebanon, India na Pakistan wote wamepigana upande wa al-Shabaab.

By Mchimba Riziki

Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score