Tuesday, July 22, 2014

Mourinho Anena Juu Ya Ujio Wa Van Gaal Manchester United. Amwambia............



Kushoto Ni Jose Mourinho akimtania Kocha Man U Van Gaal Kulia.
Kocha wa klabu ya Chelsea, Jose Mourinho, amejitanua kifua kwamba hamwogopi  mkufunzi mpya wa Manchester United, Louis Van Gaal wakati msimu mpya unapozidi kukaribia kuanza.
Wawili hao ambao ni marafiki wakubwa waliwahi kufanya kazi pamoja katika klabu ya Barcelona, Mourinho akiwa mkalimani na mwenzake kocha.

Makocha hawa wawili wana mafanikio makubwa kwenye taaluma yao ya ukufunzi  japo hawajawahi kujipata katika ushindani zaidi ya mwaka wa 2010 walipokutana kwenye fainali ya dimba la klabu bingwa Ulaya.
Wakati huo Mourinho alikuwa akiifunza Inter Milan ya Italia naye Van Gaal akinoa Bayern Munich ya Ujerumani. Timu hizo zilikutana kwenye fainali hizo na  Mourinho akaibuka kidedea kwa kutwaa ubingwa.
Mwaka huu, watagongana vichwa kwenye Ligi Kuu ya Uingereza ambapo Van Gaal ameapa kujaribu kushinda taji katika msimu wake wa kwanza akiwa uongozini huku naye mwenzake akisisitiza wazo sawa na hilo.
“Sina wasiwasi kwamba kwa sasa yupo hapa. Mwanzo ninatamani sana kukutana na United na wala sioni cha kunipa hofu. Hii ni kwa sababu sisi sote ni makocha wazuri na ninachojua ni kuwa ataisaidi Manchester United,” Mourinho alisema.
“Van Gaal kwa mtazamo wangu ndiye aliyekuwa kocha bora wa dimba la dunia na ni mtu ninayemheshimu sana kutokana na urafiki wetu mkubwa wa siku nyingi. Ila pamoja na yote, katika ushindani kila mmoja atajisimamia,” aliongeza.
Van Gaal alianza majukumu yake mapya klabuni humo juma lililopita na tayari ameapa kuirejesha United kwenye hadhi yake ya ushindani ligini baada ya kumaliza ya saba msimu uliopita chini ya ualimu wa David Moyes aliyepigwa kalamu.
Kwa sasa Van Gaal yuko na kikosi hicho jijini Miami, Marekani anakokitayarisha kwa mechi kadhaa za kirafiki. Kwa wakati huo huo anaendelea kufanya usajili ili kukirutubisha kikosi hicho hata zaidi.

Mkataba Wa Vana Gaal
Mkufunzi huyo alitia saini kandarasi ya miaka mitatu na United na mechi yake ya kwanza ya Ligi inayoanza Agosti 16, itakuwa dhidi ya Swansea siku mbili kabla ya Chelsea kuanza kampeni yao vile vile dhidi ya Burnley iliyopandishwa daraja.
Tetesi Za Usajili
Boss wa Manchester City Manuel Pellegrini anapanga kumchukua Didier Drogba, 36, ambaye pia anasakwa na klabu yake ya zamani Chelsea (Daily Star), meneja wa Manchester United Louis van Gaal anataka kutoa pauni milioni 17 kumchukua beki mkabaji wa Ajax Daley Blind, 24 (Daily Express), United pia wameripotiwa kuwa karibu kumsajili beki wa kati wa Borussia Dortmund Mats Hummels, 25, kwa pauni milioni 16 (Daily Mail), Tottenham wameambiwa watoe pauni milioni 25 kama wanamtaka kiungo wa Real Sociedad Antoine Griezmann, 23, ambaye pia anafuatiliwa na Chelsea na Monaco (Daily Telegraph), boss wa Arsenal, Arsene Wenger amesema hatosajili mshambuliaji msimu huu na hivyo kufuta tetesi zinazomhusisha na Mario Balotelli wa AC Milan (Daily Mirror), kiungo wa Ureno Thiago Mendes, 23, ametupilia mbali uwezekano wa kurejea Chelsea na angependa kusalia Atletico Madrid miaka miaka mingine miwili (Daily Express), PSG watakwepa sheria za Fifa za fedha kwa kumchukua Angel Di Maria, kwa mkopo kwa mwaka mmoja kutoka Real Madrid. Di Maria anasakwa pia na Man United (Daily Express), Arsenal, Chelsea na Man United wanamtaka beki Reece Oxford, 15, baada ya kinda huyo kuonesha kipaji msimu uliopita akiwa na West Ham ya vijana (Daily Star), Arsene Wenger atamruhusu Thomas Vermaelen kwenda Manchester United, ikiwa tu atarhusiwa kumchukua Phil Jones au Chris Smalling (Daily Mirror), Chelsea watampa Didier Drogba mkataba wa miezi 12 wa kucheza ambao hautakuwa na kipengele cha kuwa kocha, ingawa Chelsea wapo tayari kuzungumzia hilo (Daily Telegraph), mshambuliaji wa Lille Divock Origi anakwenda Boston Marekani kuungana na Liverpool ambao wapo katika ziara ya mechi za kabla ya msimu. Atafanyika vipimo kabla ya kukamilisha uhamisho wake wa pauni milioni 10. Huenda pia akarejeshwa Lille kwa mkopo (Daily Star).



0 maoni:


Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score