Monday, June 30, 2014

Pasta Mmoja Afukuzwa Kazi Kwa Kuendekeza Uhuni Mtaani.

Waumini wa kanisa moja la Kaunti ya Murang’a Jumapili walipitisha hoja ya kumtimua pasta wao baada ya  kutiwa rumande kwa madai ya kufanya uhuni katika jamii.
Pasta Simon Kanyoro wa kanisa la Revival Ministries lililoko katika Eneo bunge la Kigumo alitakiwa kwanza kushiriki kesi zake mbili zinazomkabili mahakamani bila ya kujihusisha na shughuli zozote za utumishi wa kanisa hilo.


Kwa kauli moja, waumini wa kanisa hilo walipitisha hoja hiyo kwa kuinua mikono juu, ambapo wote waliokuweko walionekana kuunga mkono pasta wao aondolewe majukumu yake na yakabidhiwe Naibu Pasta wao.

Katika kikao kilichoandaliwa katika tawi la kanisa hilo la Maragua, Kiongozi wa masuala ya ustawishaji wa Injili Bi Hellen Wangui aliwasilisha hoja hiyo kujadiliwa na baraza la wazee wa kanisa na ndipo hatima ya pasta huyo ikatolewa.

Kwa sasa, pasta huyo ako katika rumande ya jela kuu ya Murang’a baada ya kukamatwa na kufikishwa mahakamani mwishoni mwa wiki jana alipovunja masharti ya bodi aliyokuwa amepewa na mahakama kuhusu kesi nyingine iliyomkabili.

Masaibu yake yalimwandama aliposhtakiwa kati mwa mwezi huu kwa kubomoa nyumba ya ndugu yake mdogo kufuatia mzozo wa shamba.

Aidha, alidaiwa kutisha kumuua ndugu huyo na alipowasilishwa mahakamani, akawachilia kwa bodi ya Sh10, 000, kiasi alicholipa na kuachiliwa huru kesi yake iendelee akiwa hajawekwa kizuizini.

Hata hivyo, Bw Kanyoro alikamatwa tena mwishoni mwa wiki jana baada ya kumpiga mlalamishi na kisha kutangazia maafisa wa polisi waliojitokeza kutuliza hali kuwa alikuwa ameamua kumuua ndugu huyo ili kesi yake mahakamani ipate uzito.

Dhamana
Ndipo alifikishwa mahakamani na akashtakiwa upya hali ambayo ilimfanya apoteze haki yake ya kuachiliwa kwa dhamana na akawekwa rumande.

Bi Wangui alisema kuwa hali hiyo kwa sasa inazua hoja nyeti katika mwongozo wa kanisa hilo na waumini wameanza kuonyesha kutoridhishwa kwao na hali iliyokuwa ikimwandama pasta huyo.

“Imetubidi tuwasilishe hoja ya kutafuta mwelekeo wa kanisa letu kuhusu masaibu yanayomwandama pasta wetu na hatimaye imeafikiwa kuwa kwanza ajitenge na masuala ya injili kutuhusu,” akasema.

Alisema wao hawajamhukumu pasta huyo, ila tu wangetaka kwanza aendelee na kesi zake mahakamani na kisha akifaulu, arejelee majukumu yake ya kanisa.
“Lakini kwa sasa, pasta wetu amesimamishwa kujihusisha na masuala ya kanisa hadi wakati atakapomalizana na kesi zake. Ikiwa atafungwa jela, basi tutakuwa na wajibu wa kutafuta mwongozo mbadala,” akasema.



0 maoni:


Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score