Friday, August 16, 2013

Hali ya Utulivu Yarejea Cairo Misri Kuanzia jana Alhamisi

CAIRO, Misri

HALI ya utulivu ilishuhudiwa Alhamisi baada ya msako wa waasi Jumatano uliosababisha vifo vya mamia ya watu na kushtumiwa kimataifa nchini Misri.

Watu 327 walifariki wanajeshi walipovamia kambi mbili za wafuasi wa kiongozi aliyetimuliwa mamlakani, Mohammed Morsi  jijini Cairo.

Hali ya dharura ilitangazwa na marufuku ya kutotoka nje kuwekwa katika miji ya Misri.

Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Amerika, John Kerry alisema hali hiyo mbaya ni pigo kubwa kwa juhudi za maridhiano.

Mkuu wa Muungano wa Ulaya wa Sera za Kigeni, Catherine Ashton na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-moon pia walishtumu hatua ya kutumia nguvu nyingi dhidi ya wafuasi hao wa Morsi.

Jana asubuhi kulikuwa na magari machache katika barabara za katikati mwa Cairo na madaraja yanayopitia mto Nile, alisema.

Waandamanaji wamekuwa wakitaka Bw Morsi, ambaye aling’olewa mamlakani na jeshi Julai 3, arudishwe.

Kundi la Muslim Brotherhood,  ambalo liliunga mkono maandamano hayo ya kupiga kambi katika eneo la Nahda na karibu na msikiti wa Rabaa al-Adawiya, limesema kuwa idadi ya kamili ya waliouawa Jumatano ni zaidi ya 2,000.

Kulingana na serikali hiyo inayoungwa mkono na jeshi, polisi 43 ni miongoni ya waliofariki na watu wengine  2,926 walijeruhiwa.

Wadadisi wamesema kuwa Muslim Brotherhood huenda wakaendelea na maandamano yake kwa sababu wamesubiri miaka 80 kuchukua mamlakai.

“Ghasia zinachangia ukosefu wa wa udhabiti, majanga ya kiuchumi na mateso,” alisema Bw Kerry huku afisi ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ikielezea kusikitishwa na mamlaka ya Misri kuchagua kutumia nguvu ilhali idadi kubwa ya raia wa Misri wanataka nchi yao iendelee mbele kwa amani katika harakati wanazoziendesha za ufanisi na demokrasia.”

Wakati huo huo, Bi Ashton alisema kuwa ni juhudi za raia wote wa Misri na jamii ya kimataifa ambazo zitaelekeza nchi hiyo katika demokrasia.

Mkutano wa dharura

Viongozi wengine pia waliongeza sauti yao kuhusiana na yanayojiri Misri.

Waziri Mkuu wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan alitaka kuwepo kwa mkutano wa dharura wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kujadili mauaji hayo, huku Waziri Mkuu wa Uingereza  David Cameron akisema ghasia hizo hazitatatua lolote na kuna haja ya pande zote mbili kukubali kujitolea.

Hata hivyo, Waziri Mkuu wa muda wa Misri, Hazem Beblawi alitetea harakati hizo katika televisheni akisema kuwa mamlaka ililazimika kurudisha usalama.

Kufuatia ghasia hizo, Makamu wa Rais Mohammed ElBaradei alitangaza kujiuzulu kwake katika serikali hiyo ya muda akisema “ kubeba lawama hata ya tone moja la damu.”

Ripoti zilisema kuwa mikusanyiko midogo katika eneo la Nahda iliondolewa mara moja lakini mapigano yaliendelea kwa masaa kadha katika maeneo ya kambi iliyokuwa karibu na msikiti Rabaa al-Adawiya.


MCHIMBA RIZIKI (Mathayo Ngotee) KENYA

Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score