Friday, October 11, 2013

Westgate Kukarabatiwa Kwa Upya

Serikali ya Kenya imetangaza mipango ya ujenzi wa haraka wa jengo la Westgate la Nairobi baada ya sehemu ya jengo hilo kuharibiwa kwenye mashambulizi ya kigaidi yaliyofanywa na wanamgambo wa al-Shabaab mwezi uliopita.

Katika mkutano wake na wamiliki wa maduka jioni ya siku ya Jumatano (tarehe 9 Oktoba), Waziri wa Biashara wa Kenya, Phyllis Kandle, alisema anataka kuona kwamba Westage inarudi kwenye shughuli zake na akaahidi msaada wa serikali.

"Serikali ya Kenya imedhamiria kwa dhati kabisa kuhakikisha kwamba shughuli za jengo la Westgate zinarudi ndani ya kipindi kifupi kabisa kadiri inavyowezekana kupitia mfumo wa ubia kati ya sekta ya umma na ya binafsi," alisema.

"Kupitia ubia huu, tutakuwa tunajaribu kuhakikisha uwezo wa pamoja wa kuhimili kwenye uchumi ngazi ya taifa kufuatia matukio ya kusikitisha kwa kupunguza kiwango cha kuporomoka kwa biashara, imani ya wawekezaji na kupotea kwa nafasi za kazi," alisema.


Kabla ya mashambulizi hayo, jengo la Westgate lilikuwa likizalisha zaidi ya shilingi bilioni 100 (dola billion 1.2) kwa mwaka na likiwa limetoa zaidi ya nafasi 2,000 za ajira. Ripoti zinasema kwamba jengo hilo limekatiwa bima ya shilingi bilioni 6.6 (dola milioni 77), na sera ya kufidiwa madhara ya mashambulizi ya kigaidi.

Hata hivyo, bado haijawa wazi ikiwa kuna utafiti wowote uliokwishafanyika wa jengo hilo kuona ikiwa kuna madhara zaidi ya kimuundo kwenye kituo hicho cha biashara kilichosababishwa na moto na kuporomoka kwa ghorofa ya nne iliyokuwa na eneo la kuegeshea magari.

Vyanzo vilivyo karibu na uchunguzi unaoendelea vinasema itachukuwa angalau kiasi cha mwezi mmoja kusafisha kifusi, liliripoti shirika la habari la AFP. Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya limesema bado watu 39 hawajapatikana, na kuna hofu kwamba miili zaidi inaweza kupatikana kwenye mabaki ya jengo hilo.

By Mchimba Riziki


Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score