Monday, April 28, 2014

Serikali Ya Somalia Yaikemea Kenya Yasema Inataka Ufafanuzi Juu Ya....... Diplomasia Baina Ya Nchi Mbili Hizi Iko Mashakani ...

WAZIRI Mkuu wa Somalia, Bw Abdiweli Sheikh Ahmed ameitaka Serikali ya Kenya kueleza kwa nini afisa wa ubalozi wa nchi hiyo alikamatwa jijini Nairobi wiki jana. Bw Ahmed pia alionya serikali ya Kenya dhidi ya kuwanyanyasa na kuwazuilia raia wa Somalia wasio na hatia wanaoishi Kenya.
Waziri Mkuu Wa Somalia Abdiweli Sheikh Ahmed
Kuingilia kwake suala hilo kunaweza kuzua mzozo wa kidiplomasia kati ya nchi hizi mbili kufuatia kutoelewana kuhusu msako kwa polisi unaolenga mitaa wanayoishi raia wenye asili ya Kisomali.

Mamia ya maafisa wakuu wa serikali na raia wa Somalia wakiwemo wabunge wana makao jijini Nairobi.
“Serikali ya  Somalia inataka majibu rasmi kutoka kwa serikali ya Kenya kufuatia kukamatwa kwa afisa wa ubalozi wa Somalia nchini Kenya,, Siyad Mohamud Shire, ambako ni ukiukaji mkubwa wa kanuni za ulinzi za maafisa wa kibalozi,” ili

sema taarifa  kutoka ofisi ya Bw Abdiweli.
Aliongeza: “Serikali ya  Somalia imekuwa ikiwasiliana kila wakati na serikali ya Kenya kuhusu kuzuiliwa huku na inataka kuona serikali ya Kenya ikichukua kila juhudi kuhakikisha raia wa Somalia wasio na hatia wamelindwa,”
Alisisitiza kwamba ulinzi wa raia wa Somali wasio na hatia, baadhi ambao wamezuiliwa katika kambi kwenye uwanja wa michezo wa Kasarani ni muhimu.
Alisema baadhi ya raia wa Somalia wanaozuiliwa, wanatekeleza wajibu muhimu wa kujenga uchumi wa Kenya na wanapasa kutunzwa vyema.

Balozi Wa Kenya Nchini Somalia Na Rais Wa Somalia
“Serikali zetu zina tisho sawa  kiusalama, lakini kuendelea kuwazuilia raia wa Somalia kunaibua hofu na kutoaminiana ambako kutagawanya jamii zetu,” akasema.
Hii leo, balozi wa Kenya nchini Somalia Bw Josephat Maikara aliambia waandishi wa habari kwamba Bw Shire, aliyezuiliwa katika kituo cha polisi cha Kilimani Ijumaa, aliachiliwa baada ya kutambuliwa. kuwa ni balozi wa Somalia nchini.
Bw Maikara alisema kukamatwa kwa afisa huyo hakuwezi kutia doa uhusiano wa Kenya na Somalia aliosema una mizizi na hauwezi kuvurugwa na misako inayoendelea kote nchini Kenya  na hailengi raia wa nchi fulani.

0 maoni:


Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score