Thursday, November 28, 2013

Makaburi Yafukuliwa Na Maiti Waliokuwemo Kuibwa Huko Kakamega.

Wakazi katika kijiji kimoja cha Kaunti ya
Kakamega, jana asubuhi walipigwa na mshangao
baada ya watu wasiojulikana kufukua makaburi
mawili na kuiba maiti.

WAKAZI katika kijiji kimoja cha Kaunti ya
Kakamega, Jumanne asubuhi walipigwa na
mshangao baada ya watu wasiojulikana kufukua
makaburi mawili na kuiba maiti.
Wanakijiji cha Shirere walisema makaburi hayo
ni ya watu wawili wazaliwa wa Ulaya waliozikwa
mahali hapo yapata miaka 70 iliyopita.

Makaburi hayo, ambayo
yamo kwenye uwanja
wazi karibu na Shule ya
Upili ya Bishop Sulumeti
yalikuwa yametelekezwa
kwa muda mrefu.

Mzee wa kijiji, Bw Andrew
Andanyi alisema mmoja
wa watu waliozikwa mahali hapo alikuwa rubani
aliyekufa kwenye ajali ya ndege.

“Makaburi haya
yamekuwepo tangu 1940 nilipokuwa mvulana,”
alisema.

Wanakijiji walisema watu wawili wasiojulikana
walitembelea mahali hapo siku mbili kabla ya
tukio hilo.

Wezi hao waliacha chupa tupu za pombe, ishara
kwamba walikunywa pombe kabla ya kufukua
maiti hizo.

Naibu wa chifu wa sehemu hiyo, Bw Morris
Mukabane alisema tukio hilo linaendelea
kuchunguzwa.

Kwingineko, vijana waliokodishwa walifukua
maiti ya mfanyabiashara wa Nakuru ambaye
mkewe na wazazi wake wanazozania mahala
atakapozikwa.

Maiti ya Evans Bari Omuhindi ambayo ilikuwa
imezikwa kwenye makaburi ya Nakuru North
dhidi ya matakwa ya wazazi wake, ilifukuliwa
Jumatatu jioni kufuatia amri ya mahakama.

Mwanaume huyo aliyeaga dunia Novemba 1
alizikwa na mkewe Bi Jesica Kanyi lakini wazazi
wa mwenda zake na mwanamke anayedai kuwa
mkewe wa pili walienda kortini kupinga hatua
hiyo.

Watoto watatu
Walidai kwamba mwili wa marehemu ulifaa
kuzikwa katika kijiji cha Ebuskami Emanake,
nyumbani alikozaliwa katika eneo la Luanda
kulingana na mila za Waluhya.

Mamake marehemu Bi Sofia Nekesa alisema
hata kama mwanawe alikuwa akiishi mjini
Nakuru na mkewe wa kwanza na watoto wao
watatu, alikuwa pia amemuoa Bi Dinah Saisi na
wakapata naye mtoto mmoja.
Bi Saisi alikuwa
akiishi na wa wazazi wa marehemu eneo la
Luanda.

Jumanne, afisa anayesimamia kituo cha polisi
cha Nakuru Central alimwambia Hakimu Mkazi
wa Nakuru, Bi Victoria Ochanda kwamba polisi
walikuwa wameufukua mwili kama korti
ilivyoagiza.

Alisema mabaki hayo yalipelekwa kwenye
chumba cha maiti cha Manispaa ya Nakuru
ukingoja uamuzi wa korti.

Chanzo Taifa Leo

Shared by,

Mchimba Riziki.

0 maoni:


Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score