Tuesday, February 4, 2014

Vikosi Vya Usalama Vya Kenya Vyavamia Msikiti Mombasa Kenya

Masjid Mussa, msikiti katika jiji la Mombasa,Kenya, ilikuwa Jumapili (tarehe 2 Februari) eneo la makabiliano mengine kati ya vikosi vya usalama vya nchi na vijana wanaoshukiwa kuwa wenye siasa kali.

Ofisa wa polisi akielekeza kirungu kwa wanaume
waliowekwa chini ya ulinzi nje ya Masjid Mussa huko
 Mombasa tarehe 2 Februari, 2014. [Na Ivan Lieman/AFP]
Vikosi vya usalama vilivamia jengo la msikiti Jumapili jioni katika kukabiliana na kile kinachosemwa kilikuwa jitihada zilizopangiliwa za kuandikisha vijana na kutoa mafunzo kwa vijana kwenye shughuli za jihadi, Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Mombasa Robert Kitur aliiambia Sabahi.

Kati ya watu watatu waliouawa katika tukio hilo, mmoja alikuwa ofisa wa polisi ambaye alikufa kutokana na majeraha ya visu, alisema, akiongezea kwamba watu 200 walikamatwa katika mapambano hayo.

Kijana akionyesha ukaidi akiwa ameshikilia bango la jihadi
baada ya kukamatwa katika eneo la Majengo la Mombasa
tarehe 2 Februari, 2014. [Na Ivan Lieman/AFP]
Mahakama Jumatatu, iliagiza kwamba watu 129 waliokamatwa katika operesheni hiyo, ikiwa ni pamoja na wanawake watatu, kuendelea kuwa chini ya ulinzi hadi tarehe 7 Februari kutoa muda kwa polisi kukamilisha uchunguzi, Kitur alisema.

Vijana wa kiume wakiwa wamelala chini nje ya Masjid
 Mussa huko Mombasa baada ya kukamatwa tarehe 2
 Februari, 2014. [Na Ivan Lieman/AFP]
Wakati vikosi vya usalama vikielekea msikitini, vilikutana na vijana wenye silaha, mapanga na fimbo, wakikataa kuwaruhusu kuingia katika eneno hilo, kwa mujibu wa Kitur. Alisema vikosi vya usalama vilivamia msikiti huo baada ya vijana kukataa kutekeleza amri ya kujisalimisha na kuwapiga risasi maofisa polisi.

"Tuliwanyang'anya visu, fimbo na bendera zinazohusiana na al-Shabaab. Polisi walipanda kwenye minara kuondoa bendera zilizokuwa zikipepea," Kitur alisema, akiongezea kwamba iliwachukua vikosi vya usalama zaidi ya saa tano kuweka hali ya usalama katika majengo manne ya jengo la msikiti.

ABaadhi bya watu waliokamatwa wakati wa operesheni
 kwenye Masjid Mussa wakipelekwa mahakamani
Jumatatu na vikosi vya usalama (tarehe 3 Februari) katika
kitongoji cha Shanzu cha Mombasa. 
"Tulipata habari za mkutano wa Alhamisi [tarehe 30 Januari] kupitia dokezo la tahadhari kutoka katika jamii. Mkutano huo ulitangazwa pia kupitia vipeperushi na vyombo vya habari vya jamii," alisema. "Tulitoa tahadhari kwamba hatutaruhusu mkutano kama huo kwa sababu ni kinyume cha sheria."

Mkuu wa polisi wa mkoa wa Pwani Aggrey Adoli alisema vikosi vya usalama vilikuwa tayari kumaliza mara moja vurugu ili kuleta hali ya kawaida kwenye mji.

Alisema vikosi vya usalama vilikuwa katika tahadhari endapo mkutano na ulinzi wa usalama unaofuatia ulikuwa ni hila za kuvizuia vikosi vya usalama kutokana na mashambulizi ya al-Shabaab pengine popote.

"Mkutano wa watu wenye msimamo mkali ulikuwa ukiendelea tangu asubuhi. Pia tunachunguza kwamba mkutano ulifanyika Ijumaa," aliiambia Sabahi. "Tunaamini vijana walitaka kuleta hali ya vurugu idumu kwa saa au siku kadhaa au hata miezi kuleta uzingativu. Vijana waliasi agizo la vikosi vya usalama kuondoka bila ya masharti kwenye mkutano na kutawanyika."

Polisi walitaka kuutawanya mkutano kwa amani, na kuepuka kuwa na majeruhi na uharibifu kwenye sehemu takatifu, alisema.

Adoli alisema viongozi wa usalama wanapanga kufanya mkutano na wahubiri wa Kiislamu katika mkoa ili kujadili hali inayoendelea. Sehemu ya ajenda ya mkutano itakuwa kujadili uwezekano wa kufunga Masjid Mussa kwa sababu ya kutumiwa kwake na vijana na wahubiri wenye msimamo mkali kuleta vurugu nchini, alisema.
"Tunaamini kikundi cha wenye msimamo mkali kinatumia msikiti katika kujaribu kuvutia utumiaji nguvu wa usalama ambao matokeo yake unavutia upinzani dhidi ya vikosi vya usalama," alisema.

Katika kujibu uwezekano wa kufunga msikiti, Seneta wa Kaunti ya Mombasa Hassan Omar Hassan alisema Jumapili kupitia Facebook, "Nina matumaini ya dhati kwamba ripoti kama hizo sio za kweli kwa kuwa hakuna serikali inayoweza kufanya tukio kama hilo la uvunjaji mkubwa wa sheria dhidi ya dini yoyote. Kitakuwa ni kitendo cha uchokozi ambacho ninakipinga kabisa."

"Ninawaomba viongozi wote na raia wetu wote wa Mombasa kutumia jitihada zetu nzuri ili kutafuta suluhisho kwa masuala haya," alisema, akiongeza kwamba suluhisho "lazima lipatikane kwa uhusishaji na majadiliano".

Masjid Mussa unafahamika kwa kusambaza msimamo mkali na unajulikana kufuatwa mara kwa mara na wafuasi wa marehemu Aboud Rogo Mohammed aliyeuawa kwa kupigwa risasi akiendesha gari mwezi Agosti 2012, tukio ambalo lilichochea siku kadhaa za vurugu Mombasa.

Rogo na wafuasi wake mara nyingi walitumia msikiti kama mahali pa kutolea hotuba, mahubiri na mihadhara kuhusu uadilifu wa jihadi.

Uvamizi wa Msikiti wasababisha Kero




Abdi Mwashumbe, 34, mkazi wa Mombasa, alisema alikuwa ndani ya msikiti wakati makabiliano kati ya vijana na vikosi vya usalama yalipoanza.

Alisema wasiwasi ulianza kujengeka wakati maofisa wa polisi walipotumia vipaza sauti kuamrisha waumini kuondoka msikitini huku wakiinua mikono yao juu.

Amri zote zilifuatiwa na kundi la vijana ndani ya msikiti kukariri kaulimbiu za kidini, alisema.

"Baadhi ya waumini walikuwa hawajui kama mikutano ya wenye msimamo mkali ilikuwa ikiendelea katika eneo hilo," Mwashumbe aliiambia Sabahi. "Wote tuliokuwa hatuna taarifa ya chochote tulitaka kufuata amri ya polisi na kutoka nje, lakini baadhi ya vijana ndani walitutaka tuondoke."

"Ilionekana kama hali ya mateka kwa sababu tulikuwa tukitumikia kama ngao," alisema, akiongeza kwamba baada ya saa mbili alikuwa na uwezo wa "kutembea kawaida na kupenya kimyakimya kutoka nje ya msikitini".

Mwashumbe alisema kwamba muda ya saa 9 alasiri, baada ya kuondoka, alisikia bunduki na mabomu ya machozi yakirushwa.

"Ninaamini polisi watawahoji kikamilifu wale waliowakamatwa kwa sababu baadhi yao hawana hatia," alisema.

Sheikh Abdallah Kheir, imam na mhadhiri wa sosholojia katika Chu Kikuu cha Kenyatta, alishutumu matumizi ya nguvu msikitini.

Alisema mkutano msikitini ulitangazwa kama mhadhara wa dini na polisi haikuwa na sababu ya kuuvuruga.

"Msikiti ni mahali patakatifu, lakini polisi waliingia msikitini wakiwa na viatu vyao na kufyatua risasi zao na mabomu ya machozi ndani ya msikiti," aliiambia Sabahi.

Kwa mujibu wa vyanzo vya polisi, maofisa walifyatua silaha zao nje ya msikiti.

Kheir alisema serikali inapaswa kushughulikia msimamo mkali kwa kutoa fursa kwa vijana.

"Vijana wengi hawana cha kufanya na wapo hatarini kwa wanaitikadi ambao wanabadilisha mawazo yao. Serikali pia inahitaji kushughulikia uonevu wa kihistoria na kutengwa kwa vijana katika mkoa wa Pwani," alisema.

Chanzo Sabahi
Mchimba Riziki

0 maoni:


Copyright © 2014. Mchimba Riziki- All Rights Reserved

Map

Live score